WABUNGE WA CCM WAPOKEA VITISHO BUNGE LA KATIBA KAMA WATAKWENDA KINYUME NA MSIMAMO WA CHAMA CHAO MJINI DODOMA.

DODOMA.
MPASUKO miongoni mwa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba wanaotokana na Chama Cha Mapinduzi (CCM), umechukua sura mpya, baada ya kuelezwa kuwa wabunge 90 wameorodheshwa kwa lengo la kuhojiwa kwa tuhuma za kukisaliti chama.
Wajumbe hao wengi wao wakiwa ni wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, wamekuwa wakiitwa na mmoja wa viongozi waandamizi wa Serikali ya CCM na kuelezwa wazi kuwa chama hakiridhiki na mwenendo wao. http://www.mwananchi.co.tz/image/view/-/2235780/medRes/702751/-/maxh/240/maxw/460/-/yqrnbvz/-/picha_ccm.jpg
Wengi wa wajumbe hao ni wale waliotamka hadharani kuunga mkono muundo wa Muungano wa Serikali tatu, badala ya Muungano wa Serikali mbili ulioboreshwa, ambao ndiyo msimamo wa chama hicho tawala.


Wengine ni wale wanaotajwa kuunga mkono upigaji wa kura wa siri katika kupitisha vifungu vya rasimu ya Katiba Mpya, ikiwa ni kinyume na msimamo wa CCM wa kutaka kura ya wazi.


“Ni kweli hata mimi niliitwa na (akimtaja jina) na kuniambia ametumwa aniletee ujumbe kuwa niko kwenye orodha hiyo na nikiendelea na msimamo huo nitachukuliwa hatua,” alidai mbunge mmoja.


Hata hivyo, mjumbe huyo alidai kuwa kinachofanywa na CCM ni sawa na kumpa mgonjwa wa saratani dawa ya kutuliza maumivu, lakini mwishowe ugonjwa alionao uko palepale.


“Mimi msimamo wangu ambao naamini ndiyo msimamo wa wabunge wengi ni kutaka kura ya siri na Serikali tatu. Nitasimamia msimamo huo, kwani ndiyo dhamira yangu kwa masilahi ya Watanzania,” alidai.


Mbunge mwingine anayetajwa kuwapo kwenye orodha hiyo (jina tunalo) alipoulizwa jana kama ana taarifa hizo alisema, “Ni kweli kuna orodha hiyo ya wabunge 90, lakini mimi sijaulizwa chochote.”


Mbunge huyo alisema, wabunge hao 90 wamewekwa katika orodha nyeusi (Black list) iliyoandaliwa na CCM kimeandaa kama njia mojawapo ya kuwatesa kisaikolojia ili waachane na msimamo wao.


Tayari CCM kupitia kwa Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye kilishaweka wazi msimamo wake kuhusu suala la muundo wa Serikali na kutaka wajumbe wake watetee kwa nguvu zote muundo wa Serikali mbili. Nape: Huu ni uwongo. MWANANCHI

0 comments:

Copyright © 2013. MSANGIBIN ALLY - All Rights Reserved
Customized by: MSANGIYUSUPHALY | Powered by: KIINICHAHABARI
Designed by: http://kiinichahabaribongo1.blogspot.com/